MKE wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mama Mariamu Mwinyi amewataka watoto wanaolelewa katika vituo mbali mbali nchini kuwa makini na waangalifu wakati wanapokwenda na kurudi katika viwanja vya sikukuu, ili kuepukana na changamoto mbali mbali zinazoweza kuwakuta. Mama Mariamu ambae pia ni Mwenyekiti wa Taasisi ya ‘Zanzibar Maisha Bora Foundation
MKE wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mama Mariamu Mwinyi amewataka watoto wanaolelewa katika vituo mbali mbali nchini kuwa makini na waangalifu wakati wanapokwenda na kurudi katika viwanja vya sikukuu, ili kuepukana na changamoto mbali mbali zinazoweza kuwakuta.
Mama Mariamu ambae pia ni Mwenyekiti wa Taasisi ya ‘Zanzibar Maisha Bora Foundation (ZMBF) ’ ametoa wito huo kwa nyakati tofauti alipotembea vituo mbali mbali vinavyotunza na kulea watoto na kuwakabidhi zawadi za mkono wa Idd el Hajj.
Katika hafla hiyo mama Mariamu aliwakilishwa na Mtendaji Mkuu wa ZMBF Mwanaidi Mohamed Ali, ambapo alitembelea vituo vya ZASO Children Home kiliopo Founi Mambosasa, Kituo cha SOS pamoja na Kituo cha Kulelea watoto Mazizini, Mkoa Mjini Magharibi.
Alisema kuna umuhimu mkubwa kwa watoto hao kujilinda wakati wote wanapokwenda na kurudi kwenye viwanja vya sikukuu, huku akiwataka watoto wenye umri mkubwa kubeba dhima ya uangalizi kwa wale wenye umri mdogo, ili waweze kukamilisha sikukuu hiyo wakiwa salama na wazima.
Aidha, aliwatakia kheri nyingi watoto hao katika sikukuu hiyo na kusisitiza umuhimu wa kutimiza jukumu lao la kuwatii wazazi na walezi pamoja na kusoma kwa bidii.
Nae, Mkurugenzi wa Idara ya ustawi wa Ustawi wa Jamii na Wazee Abdalla Saleh Omar aliwataka watoto hao kufuata maelekezo wanayopewa na walezi wao, sambamba na kujikinga na vishawishi vyote ili waweze kufanikiwa.
Aliwakumbusha watoto hao wajibu walionao wa kuongeza bidii katika masomo yao, akibainisha hatua hiyo itawawezesha kufikia mafanikio makubwa katika siku za usoni.
Alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, awamu ya nane itaendelea kuwahudumia kikamilifu watoto wote nchini, ikiwa ni hatua ya kuendeleza utaratibu ulioasisiwa na Awamu ya kwanza ya Serikali mara baada ya Mapinduzi ya 1964.
Mkurugenzi huyo alisema kipindi hicho cha sikukuu ni wakati wa furaha kwa watoto wote, hivyo akawataka kuthamini viongozi wa Maisha Bora Foundation, chini ya Uongozi wa Mama Mariamu kwa kufika vituoni humo na kutoa mkono wa Idd el Hajj.
Aidha, Viongozi wa Vituo hivyo wamemtakia kheri na Idd njema Mama Mariamu na familia yake na kutoa shukrani za dhati na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Mwinyi kwa namna wanavyowapenda, kuwajali na kutetea maslahi ya watoto nchini kote.
Vile vile, mtoto Rauhiya Omar Ali kutoka kituo cha ZASO akitoa neno la shukrani, alimuomba Mwenyezi Mungu kumjaalia afya bora na maisha mema Mama Mariamu kwa kuwajali na kuwathamini watoto, sambamba na msaada wake uliofanikisha kituo hicho kupata leseni.
Katika hatua nyengine, wazee wanaoishi katika Vituo vya kutunza wazee vya Sebleni na Welezo nao walipatiwa zawadi hiyo ya mkono wa Eid Hajj.
Leave a Comment
Your email address will not be published. Required fields are marked with *