Na Barnabas Kisengi-Kongwa Waziri wa Kilimo Mhe. Prof. Adolf Mkenda (Mb) amesema kuwa Wizara ya Kilimo ilifanya utafiti ikagundua kuwa ili iweze kupiga hatua kubwa za kimaendeleo katika sekta ya kilimo ni wazi kuwa lazima kuwatumia maafisa ugani kwa umuhimu na ufanisi mkubwa. Amesema kuwa maafisa ugani ndio mboni ya jicho la Wizara ya Kilimo
Na Barnabas Kisengi-Kongwa
Waziri wa Kilimo Mhe. Prof. Adolf Mkenda (Mb) amesema kuwa Wizara ya Kilimo ilifanya utafiti ikagundua kuwa ili iweze kupiga hatua kubwa za kimaendeleo katika sekta ya kilimo ni wazi kuwa lazima kuwatumia maafisa ugani kwa umuhimu na ufanisi mkubwa.
Amesema kuwa maafisa ugani ndio mboni ya jicho la Wizara ya Kilimo hivyo ili nchi iweze kuwa na kilimo bora kinachokidhi matakwa ya tija na wingi wa uzalishaji na kuwa na kilimo kitakachokidhi matakwa ya soko ni wazi kuwa elimu ni muhimu itolewe kwa wakulima.
Waziri wa Kilimo ameyasema hayo leo tarehe 17 Agosti 2021 wakati akizungumza kwenye kikao kazi na maafisa ugani wa Wilaya ya Kongwa akiwa katika ziara ya kikazi ya siku moja wilayani hapo mkoani Dodoma.
Amesema kuwa serikali imeandaa mafunzo rejea kwa maafisa ugani wote nchini ili kuimarisha sekta ya kilimo na kila afisa ugani katika mikoa kielelezo ya Dodoma, Singida na Simiyu atakabidhiwa Pikipiki kwa ajili ya kurahisisha huduma zao kwa kuwafikia wakulima wengi kwa siku.
Ameongeza kuwa pamoja na pikipiki hizo kwa maafisa ugani, pia serikali itawapatia simu za mkononi kwa ajili ya kurahisisha huduma za mawasiliano na wakulima ikiwa ni pamoja na kuzitumia kwa ajili ya taarifa za utendaji kazi wao.
Pia, ameongeza kuwa maafisa ugani wote wanapaswa kuwa na mashamba ya mifano ambayo serikali itaandaa mfumo mzuri kwa ajili ya kuwasaidia pembejeo ili wawe kielelezo kizuri kwa wakulima katika maeneo yao.
“Mimi nikitaka kujua kama kweli afisa ugani anafanya kazi yake inavyotakiwa nikienda kwenye eneo lake si nitaomba tu kuona shamba lake alilolima kisha nitajiridhisha kwamba anafaa” Amekaririwa Waziri Mkenda.
Kuhusu kilimo cha alizeti Waziri Mkenda amesema kuwa maafisa ugani wengi wamekuwa wakifanya kazi zisizohusiana na kilimo lakini serikali ipo katika mkakati wa kuwarejesha kwenye majukumu yao ili kuongeza kasi ya kukuza kilimo nchini.
Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo-Kongwa.
Leave a Comment
Your email address will not be published. Required fields are marked with *