HOTUBA YA MHESHIMIWA KASSIM MAJALIWA MAJALIWA (MB.), WAZIRIMKUU WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA WAKATI WA KUAHIRISHAMKUTANO WA 13 WA BUNGE LA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA TAREHE 10 NOVEMBA, 2023 JIJINI DODOMA UTANGULIZIShukurani Check Against Delivery 2 Check Against Delivery 3 Maswali na Majibu Tatu: Muswada wa Sheria ya Bima ya Afya kwa wote
HOTUBA YA MHESHIMIWA KASSIM MAJALIWA MAJALIWA (MB.), WAZIRI
MKUU WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA WAKATI WA KUAHIRISHA
MKUTANO WA 13 WA BUNGE LA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
TAREHE 10 NOVEMBA, 2023 JIJINI DODOMA
UTANGULIZI
Shukurani
- Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa
rehema kwa kutujalia uzima na afya njema na kutuwezesha kuhitimisha shughuli zote za
Mkutano wa 13 wa Bunge la 12 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kama
zilivyopangwa. Hivyo basi, tuendelee kumuomba Mwenyezi Mungu atupe hekima na nguvu
ya kuweza kutekeleza maazimio yote yaliyopitishwa na Bunge lako tukufu. - Mheshimiwa Spika, ninamshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suhulu Hassan,
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa jitihada za kutekeleza dhamira yake ya
dhati ya kuwaletea maendeleo wananchi wa Tanzania. Sina shaka nyote mtakubaliana
nami kuwa uongozi wake makini na busara zake zimeendelea kuchagiza maendeleo ya
haraka ya uchumi wa nchi yetu pamoja na ustawi wa Mtanzania mmoja mmoja.
Ninampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoifanya, ninawasihi
Watanzania wote tuendelee kumuunga mkono ili aweze kutimiza dhamira yake. - Mheshimiwa Spika, naomba pia nitumie fursa hii kumshukuru sana Dkt. Philip
Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea
kumsaidia Mheshimiwa Rais kutelekeza majukumu yake ya kuwatumikia Watanzania.
Ninampongeza sana Mheshimiwa Makamu wa Rais kwa jitihada anazozifanya, ama kwa
hakika busara zake zimekuwa chachu katika kuleta maendeleo ya haraka ya Taifa letu. - Mheshimiwa Spika, awali ya yote nitumie fursa hii kukupongeza sana kwa
kuchaguliwa kuwa Rais wa 31 wa Umoja wa Mabunge Duniani, IPU, katika kikao cha
Baraza la Uongozi kilichofanyika tarehe 23 hadi 27 Oktoba huko Luanda, nchini Angola.
Vilevile, ninakupongeza sana kwa kuwa Rais wa Tatu mwanamke kushika nafasi hiyo
ambayo imeshawahi kushikwa na Mheshimiwa Najma Heptulla kutoka India (1999–2002)
na Mheshimiwa Gabriela Cuevas kutoka Mexico (2017–2020). Kipekee ninakupongeza
sana kwa kuwa Rais wa kwanza Mwanamke kutoka Afrika kuchaguliwa kushika nafasi hiyo
kubwa ya Rais wa Mabunge Duniani. - Mheshimiwa Spika, nirudie kukupongeza sana kwa ushindi huo ambao kwa
hakika umetuletea heshima kubwa sana Watanzania kwani umeithibitishia Dunia nzima
kuwa Watanzania tunao uwezo mkubwa wa uongozi na tunaaminika sana. Nitumie fursa
hii kukutakia kila la heri Mheshimiwa Spika katika kutekeleza majukumu yako na niwasihi
waheshimiwa wabunge wenzangu na Watanzania wote tuendelee kumwombea heri
Mheshimiwa Spika.
Check Against Delivery
2
- Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii pia kukushukuru na kukupongeza sana
kuendelea kuliongoza vema Bunge hili tukufu na kusimamia vema mijadala yote
iliyoendeshwa katika Mkutano huu wa 13 tutakaouhitimisha hivi leo. Mwenye macho
haambiwi tazama, hekima, ukomavu na weledi wako umeendelea kuongezeka siku hata
siku. Hongera sana Mheshimiwa Spika! - Mheshimiwa Spika, nimshukuru pia Mheshimiwa Mussa Azzan Zungu (Mb.),
Naibu Spika kwa kazi nzuri anayoifanya ya kukusaidia wewe Mheshimiwa Spika kutekeleza
majukumu ya kuliongoza Bunge. Vilevile, niwashukuru Waheshimiwa Wenyeviti wa Bunge
ambao ni Mheshimiwa Najma Murtaza Giga (Mb.) na Mheshimiwa Daniel Baran Sillo (Mb.). - Mheshimiwa Spika, nami niungane na Waheshimiwa Wabunge wenzangu
kumpongeza kwa dhati Mheshimiwa Bahati Ndingo, Mbunge wa Jimbo la Mbarali, kwa
kuchaguliwa kuwa Mbunge wa Jimbo hilo kufuatia uchaguzi mdogo uliofanyika hivi
karibuni. Ushindi huo wa kishindo ni kielelezo tosha kuwa wananchi wa Jimbo la Mbarali
bado wana imani kubwa kwa Serikali yao ya Chama Cha Mapinduzi. Vilevile,
ninampongeza sana Mheshimiwa Aziza Sleyum Ally kwa kuteuliwa kuwa Mbunge wa Viti
Maalum kupitia Chama cha Mapinduzi. Nitumie fursa hii kukukaribisha sana, na kwa
upande wetu, sisi Wabunge tunakuhakikishia kuwa tutakupa ushirikiano wa kutosha katika
kutekeleza majukumu yako ya kuwatumikia wananchi. - Mheshimiwa Spika, nitakuwa mchoyo wa fadhila kama sitowashukuru
Waheshimiwa Wabunge wenzangu kwa kazi kubwa mliyoifanya. Mmeshiriki kikamilifu
kutoka kamati, mijadala ambako hoja mbalimbali zilizowasilishwa wakati wa Mkutano huu.
Michango yenu ni muhimu sana katika kuimarisha ustawi na huduma kwa Watanzania.
Hivyo basi, niwahikishie kuwa Serikali imepokea michango yote, maoni pamoja na ushauri
wenu ambao kimsingi umekuwa ukisaidia sana katika kutekeleza mipango na mikakati
mbalimbali ya Serikali.
Salamu za Pole - Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Septemba hadi Novemba 2023, wapo
Watanzania wenzetu waliopatwa na majanga mbalimbali yakiwemo ajali za barabarani,
moto na mengine yaliyosababisha vifo na uharibifu wa mali. Kwa masikitiko makubwa
ninatoa salamu nyingi za pole kwa wahanga wote wa majanga hayo. Aidha, ninatoa pole
kwa ndugu, jamaa na marafiki waliopoteza wapendwa wao kutokana na masahibu hayo.
Kwa wale majeruhi tuzidi kuwaombea uponyaji wa haraka na kwa marehemu tuwaombee
kwa Mwenyezi Mungu ili azilaze roho za marehemu mahali pema peponi. Amina!
SHUGHULI ZA BUNGE - Mheshimiwa Spika, Mkutano huu wa 13 wa Bunge lako tukufu, ulipokea na
kujadili taarifa mbalimbali kutoka kwa kamati za Kudumu za Bunge, maswali kutoka kwa
Waheshimiwa Wabunge na majibu ya Serikali sambamba na kujadili na kupitisha miswada
ya sheria.
Check Against Delivery
3
Maswali na Majibu
- Mheshimiwa Spika, kupitia mkutano huu, Waheshimiwa Wabunge waliuliza
maswali 154 ya msingi na mengine 454 ya nyongeza ambayo yalijibiwa na Serikali.
Halikadhalika, maswali manne ya papo kwa papo yaliulizwa na Waheshimiwa Wabunge na
kujibiwa na Waziri Mkuu baada ya kuwa nimetoa taarifa kuhusu Kuidhinishwa kwa Sera ya
Elimu na Mafunzo 2014, Tolea la 2023 na Mitaala ya Elimu ngazi ya Elimu ya Awali,
Msingi, Sekondari na Elimu ya Ualimu mbele ya Bunge lako tukufu.
Miswada ya Sheria - Mheshimiwa Spika, katika Mkutano huu, Bunge lako tukufu limepokea Miswada
nane ya sheria kama ifuatavyo:
Moja: Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbakmbali (Na.4) wa Mwaka
2023 [The Written Laws (Miscellaneous Amendments) (No.4) Bill, 2023].
Mbili: Muswada we Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali za Sekta ya Sheria
wa Mwaka 2023 [The Legal Sector Laws (Miscellaneous Amendments) Bill,
2023]
Tatu: Muswada wa Sheria ya Bima ya Afya kwa wote wa Mwaka 2023.
Nne: Muswada wa Sheria ya Uwekezaji wa Umma wa Mwaka 2023.
Tano: Muswada wa Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani wa Mwaka
2023.
Sita: Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (5) wa Mwaka
2023(The Written Laws Miscellaneous Amendments) (No.5) Bill, 2023.
Saba: Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria za Vyama vya Siasa wa Mwaka
2023 (The Political Affairs Laws (Ammendment) Bill, 2023.
Nane: Muswada wa Sheria ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi wa Mwaka 2023.
Maazimio ya Bunge
- Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Kanuni ya 61 na 107 hadi 112 za Kanuni za
Kudumu za Bunge Toleo la Februari 2023, na kwa kuzingatia wajibu wa Bunge katika
kuisimamia na kuishauri Serikali, Bunge lako tukufu lilipokea, kujadili na kupitisha
Maazimio mawili kama ifuatavyo:
Check Against Delivery
4
Moja: Azimio la Bunge kuhusu Mapendekezo ya Kuridhia Mkataba wa Kuanzisha Taasisi
ya Dawa ya Afrika la Mwaka 2023 (Treaty for Establishment of the African
Medicines Agency – AMA).
Mbili: Azimio ta Bunge kuhusu Mapendekezo ya Tanzania Kundhia Kusunga na Mkataba
we Wakala wa Kimataifa wa Nishati Jadidifu la Mwaka 2009 (Statute of the
Intemational Renewable Energy Agency – IRENA).
- Mheshimiwa Spika, Maazimio haya yalipokelewa na kujadiliwa na Waheshimiwa
Wabunge kwa ustadi wa hali ya juu huku wakionesha nia njema ya kujenga mustakabali
mwema wa taifa letu. Kwa dhati niwapongeze Waheshimiwa Wabunge kwa kukubali
kuridhia kupitisha maazimio haya.
Taarifa za Serikali Bungeni - Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Kanuni ya 56 ya Kanuni za Kudumu za Bunge
Toleo la Februari 2023, Bunge lako tukufu katika Mkutano wa 13 lilipokea Taarifa ya
Serikali kuhusu Kuidhinishwa kwa Sera ya Elimu na Mafunzo 2014, Tolea la 2023 na
Mitaala ya Elimu ngazi ya Elimu ya Awali, Msingi, Sekondari na Elimu ya Ualimu niliyoitoa
mbele ya Bunge lako Tukufu siku ya tarehe 3 Novemba 2023.
Taarifa ya Kamati za PAC na LAAC kuhusu hesabu zilizokaguliwa na CAG kwa
mwaka wa fedha 2021/2022 na Taarifa ya Kamati ya PIC kuhusu Uwekezaji
na Mitaji ya Umma kwa mwaka wa fedha 2021/2022 - Mheshimiwa Spika, Mkutano huu wa 13 wa Bunge lako ulipata nafasi pia ya
kupokea na kujadili kwa kina Taarifa za Kamati za Bunge ikiwemo Kamati ya Kudumu ya
Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za
Mitaa (LAAC), na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) kwa
Mwaka wa Fedha 2021/2022 ulioishia tarehe 30 Juni, 2022. Taarifa hizi za Kamati
zinazotokana na Taarifa za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali. - Mheshimiwa Spika, taarifa za Kamati hizi tatu zimechambua kwa kina hoja
mbalimbali za ukaguzi zinazohusu matumizi ya fedha za umma kwa hesabu za Serikali
Kuu, Mamlaka za Serikali za Mitaa, Mashirika ya Umma pamoja na mwenendo wa
uwekezaji wa mitaji ya umma uliofanywa na taasisi za umma kwa mwaka wa fedha
ulioiishia tarehe 30 Juni, 2022. Jumla ya maazimio 117 yaliyotokana na hoja 14
yameweza kutolewa na Bunge, ambayo kimsingi ni maelekezo mahsusi kwa Serikali. - Mheshimiwa Spika, niruhusu nitoe pongezi za dhati kwa ndugu Charles E.
Kichere, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali pamoja na Ofisi ya Taifa ya
Ukaguzi kwa kuendelea kuwa taasisi yenye kuaminika inayotoa Huduma za Ukaguzi kwa
kuzingatia viwango vya kimataifa. Nyote ni mashahidi kwamba, ofisi hii imendelea
kujipambanua kwa namna inavyojenga, inavyokuza na kuimarisha utamaduni wa
uwajibikaji katika kusimamia na kudhibiti ipasavyo ukusanyaji wa mapato na matumizi ya
Check Against Delivery
5
Serikali kama inavyoidhinishwa na Bunge katika Wizara na Taasisi za Serikali, Mikoa na
Halmashauri. Vilevile, Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi imeweza kuwahikikishia Watanzania na
jamii yote namna ambavyo nchi yetu inavyoweza kupata faida au tija kutokana na
matumizi bora ya fedha za Umma, na namna ambavyo mali za Umma zinahifadhiwa,
kutunzwa na kulindwa ipasavyo.
- Mheshimiwa Spika, niwashukuru Maafisa Masuuli pamoja na Watendaji wote
wa Serikali kwa namna ambavyo wameweza siyo tu kujibu hoja za Ukaguzi ambazo
zilibainishwa katika Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, lakini pia
kuweza kutekeleza takwa la Kikatiba la kufika mbele ya Kamati husika za Bunge kwa ajili
ya ufafanuzi wa kina. Aidha, nitoe shukrani zangu kwa Waheshimiwa Mawaziri kwa
michango yao katika kutoa majibu ya Serikali kwa baadhi ya hoja zilizoibuliwa na
Waheshimiwa Wabunge. Ni ukweli ulio bayana kwamba hoja zilizoibuliwa na
Waheshimiwa Wabunge ni nyingi, muhimu na zote zinahitaji majibu na utekelezaji wa
haraka. Niseme tu kuwa Serikali yenu ni sikivu na itatekeleza mapendekezo hayo kwa
kutoa majibu sahihi na utekelezaji wa haraka. - Mheshimiwa Spika, hivyo basi, niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge pamoja
na majibu yaliyotolewa na Serikali, mturuhusu tufanyie kazi masuala yote yanayohitaji
mabadiliko ya kisera na kisheria. Na mabadiliko haya yote tutalishirikisha kikamilifu
Bunge hili ili kutimiza ndoto na malengo ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kuwaletea Watanzania maendeleo endelevu. - Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kulihakikishia Bunge lako Tukufu kuwa
Serikali baada ya kupokea hoja na maazimio yote, tayari imeandaa Bangokitita ambalo
linaainisha jukumu la kila Wizara kwa ajili ya kufanyia kazi maelekezo ya Bunge ili
kurahisisha uwasilishaji wa taarifa ya utekelezaji kwa waheshimiwa wabunge rejea yao.
Hivyo basi, ninaziagiza Wizara husika ziandae kwa wakati taarifa za utekelezaji wa
Maazimio yote kulingana na mapendekezo yaliyotolewa na Kamati. Ofisi ya Waziri Mkuu
kwa upande wake, itaandaa taarifa ya Serikali ambayo itawasilishwa kwa Mheshimiwa
Spika.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha
2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na
Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 - Mheshimiwa Spika, pamoja na hoja za Kamati za Bunge zilizopokelewa na
kujadiliwa na Waheshimiwa Wabunge, Serikali iliwasilisha Mpango wa Maendeleo wa
Taifa na Maandalizi ya Mpango na Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025
ambapo Waheshimiwa Wabunge wameweza kuchangia hoja hii moja kwa moja na kwa
maandishi. Ninawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa michango yao katika
Mpango huu pamoja na Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti kwa mwaka
2024/2025.
Check Against Delivery
6
- Mheshimiwa Spika, ikumbukwe kwamba Mipango ya Maendeleo ya kila mwaka
ni nyenzo muhimu ya matumizi bora ya rasilimali kwa ajili ya maendeleo ya wananchi.
Mipango hii huhakikisha malengo ya Dira 2025 yanafuatiliwa na kusimamiwa kila mwaka
ili kuweza kukuza uchumi na kuondoa umaskini nchini. Mapendekezo ya Mpango
yameainisha maeneo mahsusi ya kipaumbele yatakayozingatiwa katika maandalizi ya
Mpango na Bajeti ya mwaka 2024/2025 kwa kuzingatia rasilimali zilizopo. - Mheshimiwa Spika, kwa ujumla katika mwaka 2024/2025 msisitizo utawekwa
katika kuchochea shughuli mbalimbali za kiuchumi; kuimarisha ushiriki wa Watanzania
katika shughuli mbalimbali za kiuchumi na maendeleo. Vilevile, msisitizo utawekwa
katika kuimarisha ushiriki wa sekta binafsi katika maandalizi na utekelezaji wa mipango,
uwekezaji na uzalishaji nchini. - Mheshimiwa Spika, Serikali pia imewasilisha Mwongozo wa Maandalizi ya
Mpango na Bajeti kwa mwaka 2024/2025. Mwongozo huu kimsingi ni maelekezo ya
jumla na maelekezo mahsusi yanayopaswa kuzingatiwa na Maafisa Masuuli katika hatua
zote za uandaaji, uwasilishaji, utekelezaji, ufuatiliaji na tathmini pamoja na utoaji wa
taarifa za utekelezaji wa mpango na bajeti kwa mwaka 2024/2025. - Mheshimiwa Spika, Mwongozo huu umejikita katika kuhakikisha Serikali
inatekeleza vipaumbele vilivyoainishwa katika Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka
Mitano 2021/2022 – 2025/2026 ambavyo ni pamoja na: kuchochea uchumi shindani na
shirikishi; kuimarisha uwezo wa uzalishaji viwandani na utoaji huduma; kukuza
uwekezaji na biashara; kuchochea maendeleo ya watu na kuendeleza rasilimali watu. - Mheshimiwa Spika, niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa michango
yao kwenye hoja hizi mbili ambazo kwa pamoja zinatoa mwelekeo wa wapi nchi yetu
inataka kufika kwa kuangalia kule tulipotoka. Hivyo, nitoe rai kwa Maafisa Masuuli na
watendaji wote wa Serikali kutafsiri kwa vitendo na kwa umakini mkubwa maelekezo
yote yaliyotolewa na Bunge hili ikiwa ni sehemu ya kutimiza ndoto za Mheshimiwa Dkt.
Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
MASUALA YA UTABIRI WA HALI YA HEWA - Mheshimiwa Spika, sote tunatambua kuwa, mvua zimeanza kunyesha katika
maeneo mbalimbali hapa nchini. Na tayari Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania imeshatoa
utabiri wa mwelekeo wa mvua za msimu wa vuli kwa kipindi cha mwezi Oktoba hadi
Desemba 2023. Utabiri huo, umebainisha uwepo wa hali ya El Nino ambayo itaambatana
na mvua kubwa na kusababisha mafuriko ambayo yanaweza kuleta athari mbalimbali
zikiwemo; madhara ya kiafya, kiuchumi, kijamii, upotevu wa mali na uharibifu wa
miundombinu. - Mheshimiwa Spika, taarifa ya utabiri wa hali ya hewa inaonesha mvua hizo
zitakuwa juu ya wastani katika maeneo mengi ya mikoa ya Kagera, Geita, Mwanza,
Manyara, Arusha, Kilimanjaro, Shinyanga, kusini mwa Mkoa wa Simiyu, kaskazini mwa
Check Against Delivery
7
Mkoa wa Kigoma, Dar es Salaam, Tanga, Pwani (ikiwemo visiwa vya Mafia) na kaskazini
mwa Mkoa wa Morogoro.
- Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kuchukua hatua stahiki kuzuia na
kupunguza madhara yanayoweza kusababishwa na uwepo wa El Nino sambamba na
kujiandaa kukabiliana na mvua hizo kubwa. Kwa msingi huo, nitumie fursa hii
kuzielekeza Wizara, Mikoa na Taasisi za Serikali kuzingatia masuala yafuatayo:
Moja: Kuainisha na kuandaa rasilimali za kujiandaa, kuzuia na kukabiliana na maafa
endapo yatatokea;
Mbili: Kuelimisha na kuhimiza wananchi kuhama kwenye maeneo hatarishi na
kuchukua tahadhari ili kuokoa maisha na mali;
Tatu: Idara na Taasisi zinazohusika na mazingira na miundombinu zihakikishe
barabara zinapitika wakati wote, mitaro na makalvati yanaimarishwa na
kusafishwa ili kuruhu maji yapite;
Nne: Sekta za maji, umeme na mawasiliano ziweke mipango ya kuzuia madhara na
kuhakikisha uharibifu katika huduma hizo unapewa ufumbuzi mapema;
Tano: Kushirikisha wadau wa maafa ikiwemo wananchi, taasisi za umma na sekta
binafsi katika mipango yote ya usimamizi wa maafa;
Sita: Kutoa taarifa haraka kwa mamlaka husika inapotokea maafa katika sekta
husika;
Saba: Kamati za Maafa katika ngazi ya Kijiji, Wilaya, Mkoa na Taifa zijipange kikamilifu
kukabiliana na changamoto za El Nino endapo zitajitokeza;
Nane: Wizara, Idara, Taasisi, Mikoa na Halmashauri ziandae mipango ya utekelezaji
katika maeneo yao kwa kuzingatia Mpango wa Taifa wa Dharura wa Kukabiliana
na Madhara ya El Nino.
- Mheshimiwa Spika, niwasihi wananchi wote kujenga utamaduni wa kufuatilia
taarifa za utabiri wa hali ya hewa na kutekeleza maelekezo yanayotolewa na Viongozi na
Mamlaka ya Hali ya Hewa ikiwemo kuhama kwenye maeneo hatarishi na kufanya
shughuli za kiuchumi na kijamii katika maeneo salama. Kwa upande mwingine, wananchi
waendelee kuweka akiba ya chakula na kutumia mvua hizo nyingi kulima mazao
yanayostawi katika mazingira ya maji mengi.
HALI YA UKUSANYAJI WA MAPATO - Mheshimiwa Spika, uchumi wa Tanzania umeendelea kuimarika kutokana na
hatua mbalimbali zinazochukuliwa na Serikali ya Awamu ya Sita ikiwemo kuwezesha
Check Against Delivery
8
uwekezaji wa kimkakati katika sekta za uzalishaji, huduma za jamii na miundombinu.
Ukuaji huo wa uchumi umechangia kuongezeka kwa uzalishaji katika sekta rasmi na isiyo
rasmi na hivyo, kuiwezesha Serikali kukusanya mapato zaidi.
- Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha robo ya kwanza ya mwaka 2023/2024,
mapato kutoka vyanzo vyote vya ndani na nje yalifikia shilingi trilioni 9.06, sawa na
asilimia 89.6 ya lengo la kipindi hicho. Kati ya kiasi hicho, mapato ya ndani yalikuwa
shilingi trilioni 6.94 sawa na asilimia 96.2 ya lengo la kipindi hicho. Mapato ya ndani
yanajumuisha shilingi trilioni 6.15 zilizokusanywa na Mamlaka ya Mapato Tanzania;
shilingi bilioni 491 za mapato yasiyo ya kodi yanayokusanywa na Wizara, Idara
zinazojitegemea na Taasisi; na shilingi bilioni 299 kutoka vyanzo vya Mamlaka za Serikali
za Mitaa. - Mheshimiwa Spika, kuongezeka kwa mapato kunatokana na juhudi kubwa
zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita, ikiwemo kuimarisha mifumo ya ukusanyaji
wa mapato na kurahisisha ulipaji wa kodi. Katika hatua nyingine, kuimarika kwa mapato
kumewezesha Serikali kuendelea kuwahudumia wananchi kupitia ujenzi na uboreshaji wa
miundombinu mbalimbali ikiwemo ujenzi wa hospitali na vituo vya afya. - Mheshimiwa Spika, vilevile, mapato hayo yamewezesha ujenzi wa reli ya kati
kwa kiwango cha kimataifa; Mradi wa Kufua Umeme wa Maji wa Julius Nyerere;
uboreshaji wa miundombinu ya barabara na reli; mpango wa Elimumsingi na Sekondari
bila ada; kuboresha Shirika la Ndege la Tanzania; usambazaji umeme vijijini na mikopo
ya wanafunzi wa elimu ya juu. - Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ili
kuhakikisha kuwa malengo ya makusanyo na utekelezaji wa bajeti kwa ujumla
yanafikiwa. Mikakati hiyo ni pamoja na: kuimarisha mifumo ya usimamizi na ukusanyaji
wa mapato; kuimarisha doria maeneo ya mipakani; kutoa elimu kwa walipa kodi kuhusu
umuhimu wa kulipa kodi kwa hiari; kuhimiza matumizi ya stakabadhi za kielektroniki za
EFD na kuendelea kuboresha mazingira ya kuvutia uwekezaji na biashara. - Mheshimiwa Spika, vilevile, mikakati hiyo inalenga kuhakikisha taasisi zenye
sura za utoaji wa huduma kwa pamoja zinaboresha mifumo ya ukusanyaji kwa
kuwezesha kutoa namba ya malipo jumuishi ili kurahisisha ulipaji kodi, ada na tozo
mbalimbali kwa wateja na hivyo kuongeza uhiari wa ulipaji kodi; na kuendelea
kusimamia na kutekeleza kikamilifu sera za bajeti na fedha. - Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kuzielekeza Mamlaka za Serikali za Mitaa
kuendelea kuboresha mifumo ya ukusanyaji wa mapato na kuimarisha mifumo ya
udhibiti wa ndani ili kuondoa mianya ya uvujaji wa mapato. Aidha, Mamlaka hizo
ziimarishe ushirikiano na Taasisi nyingine za umma kwenye ukusanyaji wa mapato
ikiwemo Mamlaka ya Mapato Tanzania.
Check Against Delivery
9
- Mheshimiwa Spika, kwa namna ya kipekee niwashukuru wananchi kwa
kushirikiana na Serikali katika ukusanyaji wa mapato ambayo ndiyo msingi wa
maendeleo yetu. Vilevile, niwapongeze kwa dhati watumishi wa taasisi zenye dhamana
na ukusanyaji wa mapato zikiwemo Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na Mamlaka za
Serikali za Mitaa kwa kufanikisha ukusanyaji wa mapato ya Serikali. Aidha, niwasihi
watumishi wote waliopewa dhamana hiyo kutekeleza jukumu hilo kwa uadilifu na
kuendelea kutoa elimu ya mlipakodi ili kufanikisha ulipaji wa kodi kwa hiyari
USIMAMIZI WA ELIMUMSINGI - Mheshimiwa Spika, sote tunafahamu kuwa mojawapo ya malengo ya elimu
nchini Tanzania ni kutoa elimu bora itakayowajengea uwezo wahitimu kushiriki kikamilifu
katika shughuli za kiuchumi. Hatua hiyo itawezesha Taifa letu kufikia uchumi wa viwanda
ifikapo mwaka 2025. - Mheshimiwa Spika, Serikali katika kutekeleza azma hiyo, imekuwa ikifanya
jitihada mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuendelea kuboresha miundombinu; kutekeleza
mpango wa elimumsingi na kidato cha tano na sita bila ada; kuongeza ajira za walimu
na wakufunzi wenye sifa; kutoa ufadhili na mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu na
maboresho ya sera na mitaala. - Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kusimamia uandikishaji wa wanafunzi
kuanzia ngazi ya elimu ya awali bila kusahau watoto wenye mahitaji maalum ambapo
zoezi ambalo huanza mwezi Oktoba kila mwaka. Kwa mwaka 2024, Serikali inatarajia
kuandikisha Watoto wa Elimu ya Awali 1,877,484 wenye rika lengwa wakiwemo
wavulana 934,560 na wasichana 942,924 na Darasa la Kwanza 1,729,180 wakiwemo
wavulana 860,870 na wasichana 868,310. - Mheshimiwa Spika, hadi sasa jumla ya watoto wa elimu ya awali 407,138 sawa
na asilimia 21.7 wakiwemo wavulana 201,244 na wasichana 206,253 wameandikishwa.
Kati ya watoto wa elimu ya awali walioandikishwa watoto wenye mahitaji maalum ni 960
kati yao wavulana ni 488 na wasichana ni 472. - Mheshimiwa Spika, watoto wanaotarajia kujiunga darasa la kwanza
walioandikishwa ni 593,452 sawa na asilimia 34.3 wakiwemo wavulana 293,728 na
wasichana 299,724. Kati ya wanafunzi wa darasa la kwanza walioandikishwa wenye
mahitaji maalum ni 1,365 wakiwemo wavulana ni 733 na wasichana 632. - Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kuwaelekeza Wakuu wa Mikoa yote nchini
kusimamia zoezi la uandikishaji katika maeneo yao ambalo itakuwa vema likihitimishwa
tarehe 31 Desemba 2023. Nitumie fursa hii pia kuwakumbusha wazazi/walezi wote
wenye Watoto wenye rika lengwa kuwaandikisha Watoto hao ili waweze kuanza masomo
ifikapo Januari, 2024.
Check Against Delivery
10
- Mheshimiwa Spika, ninatoa wito kwa wadau wote wa maendeleo zikiwemo
Taasisi za Kidini na Taasisi za Kiraia kushiriki katika kutoa hamasa kwa Watanzania nchi
nzima ili watoto wote wenye rika lengwa waweze kuanza masomo mwezi Januari. - Mheshimiwa Spika, jitihada hizo zinaenda sambamba na kukamilisha
maandalizi yote muhimu ya kuwapokea wanafunzi wa kidato cha kwanza mwaka 2024
ikiwemo ujenzi wa miundombinu. Jumla ya wanafunzi 1,206,995 sawa na asilimia 86.4
ya wanafunzi 1,397,370 waliosajiliwa kufanya mtihani wa kuhitimu Elimu ya Msingi
mwaka 2023 wanatarajiwa kujiunga na Elimu ya Sekondari Januari, 2024. - Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kuwakumbusha Waheshimiwa Wakuu wa
Mikoa wote nchini wahakikishe kuwa ujenzi wa miundombinu yote katika Shule za
Sekondari unakamilika kabla ya tarehe 30 Novemba 2023. Serikali itachukua hatua kali
kwa wote watakaoshindwa kukamilisha ujenzi wa miundombinu katika Shule za
Sekondari. Wakuu wa Mikoa fanyeni ufuatiliaji, Serikali imeshapeleka fedha kwa ajili ya
ujenzi katika Halmashauri zote nchini hivyo hakuna sababu wala visingizio vya
kutokamilisha ujenzi kwa wakati.
MIKOPO YA ELIMU YA JUU - Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kuongeza fursa za upatikanaji wa elimu
ya kati na ya juu kwa kuwezesha vijana wa Kitanzania kupata mikopo ya wanafunzi.
Katika mwaka wa masomo 2023/2024 Serikali imetenga shilingi bilioni 786 kwa ajili ya
mikopo na ruzuku kwa wanafunzi wa vyuo vikuu na vyuo vya kati. - Mheshimiwa Spika, kati ya fedha hizo shilingi bilioni 731.3 zitatolewa kama
mikopo kwa wanafunzi 220,376 wa shahada mbalimbali; shilingi bilioni 6.7 kwa
wanafunzi 1,200 wanaofadhiliwa kwa mpango wa Samia Scholarship; na shilingi bilioni
48 kwa wanafunzi wa stashahada zenye uhitaji mkubwa wa rasilimaliwatu nchini. - Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuongeza wigo wa utoaji wa mikopo
kwa wanafunzi ambapo katika mwaka wa masomo 2023/2024 utoaji wa mikopo
umehusisha wanafunzi wa stashahada. Dirisha la kupokea maombi ya mkopo kwa
wanafunzi wa stashahada lilifunguliwa tarehe 7 Oktoba 2023 na kufungwa tarehe 29
Oktoba 2023. Hadi dirisha linafungwa jumla ya waombaji 12,910 walikuwa
wamewasilisha maombi. - Mheshimiwa Spika, kwa upande shahada hadi tarehe 5 Novemba 2023 jumla
ya wanafunzi 169,180 sawa na asilimia 77 ya lengo walikuwa wamepangiwa mikopo
yenye thamani ya shilingi bilioni 555.8. Kati yao, wanafunzi 73,078 ni wapya wa shahada
za kwanza na wengine 96,102 ni wanufaika wanaoendelea na masomo ambao matokeo
yao ya ufaulu wa mitihani na kuendelea na masomo yamepokelewa na Bodi ya Mikopo. - Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kuiagiza Wizara ya Elimu, Sayansi ya
Teknolojia kusimamia kikamilifu zoezi la utoaji wa mikopo na kuhakikisha kuwa zoezi hilo
Check Against Delivery
11
linakamilika kwa wakati sambamba na kushughulikia kwa wakati changamoto za utoaji
wa mikopo kwa wanafunzi pale zinapojitokeza.
- Mheshimiwa Spika, pamoja na Serikali kutoa fedha nyingi kuwawezesha vijana
wa Kitanzania kupata elimu ya juu, bado kuna baadhi ya waajiri na wanufaika wa
mikopo ambao hawatimizi wajibu wao wa kurejesha fedha waliokopeshwa ili mfuko
uweze kusomesha vijana wengi zaidi. Hivyo basi, nitoe wito kwa waajiri na wanufaika
wadaiwa wote kutimiza wajibu wao wa kisheria wa kurejesha mikopo hiyo kwa hiyari.
KUIMARISHA MAZINGIRA YA BIASHARA - Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji ili
kuimarisha na kuvutia wawekezaji wa ndani na nje ya nchi. Sote tumeshuhudia
mabadiliko ndani ya Serikali yaliyofanywa na Mheshimiwa Rais, kwa kuanzisha Ofisi ya
Rais, Mipango na Uwekezaji ili kuimarisha uratibu na kuongeza imani zaidi kwa
wawekezaji. - Mheshimiwa Spika, ili kuendelea kuimarisha uwekezaji nchini ninaomba nitumie
fursa hii kusisitiza masuala yafuatayo:
Moja: Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji kupitia Kituo cha Taifa cha Uwekezaji (TIC)
kwa kushirikiana na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, NIDA,
BRELA, TRA, Idara ya Kazi, Idara ya Uhamiaji, NEMC, TANESCO, TBS, OSHA na
TMDA, iboreshe mwongozo wa uwekezaji ili kubainisha fursa kulingana na
mazingira ya sasa na kuzingatia taratibu za kuwatambua na kuwasajili
wanaotaka kuwekeza nchini;
Mbili: Kituo cha Taifa cha Uwekezaji (TIC) kiimarishe matumizi ya TEHAMA ili
kutangaza fursa nyingi za uwekezaji zilizopo nchini na kuwawezesha wawekezaji
kutumia TIC kama kiungo cha kupata taarifa muhimu kutoka kwenye taasisi za
Serikali nchini; na
Tatu: TIC ihakikishe kuwa mwongozo wa uwekezaji unapatikana kwa urahisi kwa
wawekezaji wa ndani na nje ya nchi.
MASUALA YA MAENDELEO YA VIJANA
- Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kuratibu shughuli za Maendeleo ya
vijana sambamba na kuandaa mfumo wa kitaifa wa uratibu wa afua zinazotekelezwa na
Wadau mbalimbali. Mfumo huo utasaidia upatikanaji wa taarifa sahihi kwa wakati na
kuwawezesha vijana kutumia fursa zilizopo kujikwamua kiuchumi. - Mheshimiwa Spika, aidha, Serikali kupitia Programu ya Ukuzaji Ujuzi imetoa
mafunzo kwa vijana 121,898. Katika kipindi cha 2017 hadi 2023 vijana 91,106 wamepata
ujuzi kwa njia ya uanagenzi. Vilevile, vijana 22,296 wamerasimishiwa ujuzi uliopatikana
Check Against Delivery
12
katika mfumo usio rasmi. Licha ya hayo, vijana 6,300 wamepata mafunzo ya uzoefu
kazini na vijana 2,196 waliokuwa kazini wameongezewa ujuzi. Pia, kupitia Mpango wa
Jenga Kesho iliyobora vijana 812 wamedahiliwa na wanashiriki mafunzo ya Kilimo
Biashara.
- Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali kupitia Mfuko
wa Maendeleo ya Vijana imetoa mikopo ya shilingi bilioni 1.88 kwa miradi 85 yenye
vijana 595. Aidha, katika mwaka wa fedha 2023/2024 Serikali imeendelea kutoa mikopo
ambapo hadi kufikia Oktoba 2023 shilingi bilioni 1.27 zimetolewa kwa miradi 56 yenye
vijana 392.
BARAZA LA TAIFA LA BIASHARA - Mheshimiwa Spika, kwa kutambua umuhimu wa Sekta Binafsi, Serikali
imeendelea kuweka mazingira wezeshi na kutengeneza fursa ya majadiliano kati ya Sekta
Binafsi na Sekta ya Umma kupitia Baraza la Taifa la Biashara. Baraza hilo huandaa vikao
vya majadiliano rasmi kufikia muafaka kati ya sekta hizo kuhusu maboresho ya mazingira
ya biashara, uwekezaji na uchumi kwa ujumla. - Mheshimiwa Spika, kutokana na jitihada hizo baraza limeongeza ushiriki wa
Sekta Binafsi kupitia mfumo rasmi na jumuishi wa majadiliano katika ngazi zote za
utawala. Vilevile, Baraza limewezesha Mikoa 11 kuratibu na kufanya mikutano ya
Mabaraza ya Biashara ya Mikoa na Wilaya. - Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa maazimio ya Baraza umewezesha kufanya
mapitio sera, sheria, kanuni, taratibu na mifumo mbalimbali; kuunganisha majukumu ya
taasisi yanayoingiliana; kuimarisha vituo vya huduma za mahali pamoja; kuanzisha na
kuunganisha mifumo ya TEHAMA na kuimarisha na kuongeza ushiriki wa Watanzania
kwenye shughuli za kiuchumi hususan miradi mikubwa inayotekelezwa na Serikali.
MKAKATI WA KUENDELEZA WANANCHI KIUCHUMI - Mheshimiwa Spika, pamoja na jitihada zilizochukuliwa na Serikali katika kutoa
mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu, ikiwa ni sehemu ya uwezeshaji kwa wananchi
wetu, Serikali inaendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya kuwaendeleza wananchi
kiuchumi. - Mheshimiwa Spika, Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC)
ambalo limeanzishwa chini ya Sheria ya Taifa ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi Na. 16
ya mwaka 2004. Sambamba na kusimamia utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Uwezeshaji
Wananchi Kiuchumi ya mwaka 2004, limepewa dhamana ya kuratibu, kufuatilia na
kusimamia utekelezaji wa shughuli zote za uwezeshaji wananchi kiuchumi ambazo ni
mtambuka na zenye kuhusisha wadau wa sekta mbalimbali za kiuchumi.
Check Against Delivery
13
- Mheshimiwa Spika, hadi kufikia Septemba, 2023, mifuko na programu za
uwezeshaji ilifanikiwa kutoa mikopo yenye thamani ya shilingi bilioni 743.7 kwa
wanufaika wapatao 6,064,957 ambapo wanawake ni asilimia 54. Aidha, kwa mwaka
2022/2023, mifuko na programu za uwezeshaji ilitoa mikopo yenye thamani ya shilingi
bilioni 743.7 ikilinganishwa na shilingi bilioni 713.8 zilizotolewa mwaka 2021/2022. Hii ni
sawa na ongezeko la asilimia 4.02.
UHUSIANO WA KIDIPLOMASIA - Mheshimiwa Spika, katika kuimarisha na kuchochea shughuli za maendeleo
nchini, Serikali imeendelea kuimarisha uhusiano wa kikanda na kimataifa kwa lengo
kufungua fursa mbalimbali ikiwemo uwekezaji na mitaji katika sekta za utalii na
uchukuzi. Katika hili, nimpongeze kwa dhati Mwanadiplomasia namba moja, Mheshimiwa
Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuwa mstari
wa mbele kuimarisha diplomasia ya uchumi. - Mheshimiwa Spika, masuala yanayozingatiwa kwenye diplomasia ya uchumi ni
pamoja na kutafuta masoko ya bidhaa zetu, kutafuta fursa za kiuchumi katika sekta
mbalimbali, fursa za elimu, mafunzo, utaalamu na ujuzi pamoja na ajira nje ya nchi na
kubidhaisha lugha ya Kiswahili. - Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha 2022/2023, Serikali iliratibu na
kufanikisha kusainiwa kwa mikataba 13 na Hati za Makubaliano 37. Mikataba na hati hizo
zinagusa sekta za kiuchumi na kijamii ikiwemo ulinzi na usalama, kilimo na uvuvi,
viwanda, biashara, uwekezaji, TEHAMA na utalii. Nyingine ni afya, elimu, uchukuzi,
mawasiliano, utamaduni, sanaa na michezo, sayansi na teknolojia, mazingira na uchumi
wa buluu. - Mheshimiwa Spika, ziara zinazofanywa na Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu
Hassan na viongozi wengine zimekuwa chachu ya kuimarisha uhusiano wa kimataifa.
Vilevile, ziara hizo zimeibua fursa zenye manufaa ya kiuchumi nchini. Baadhi ya
mafanikio yaliyopatikana hadi sasa ni ongezeko la watalii, ongezeko la wafanyabishara
na wawekezaji, miradi mikubwa na ya kati, uwekezaji na kufungua masoko ya bidhaa
mbalimbali. Kipekee, nimpongeze tena Mheshimiwa Rais wetu ambaye kupitia ziara zake
na nchi jirani, aliweza kutatua changamoto za kibiashara kwenye mipaka ya Kenya na
Zambia. - Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuratibu na kufanikisha ziara za kikazi
na kitaifa za Viongozi Wakuu kutoka mataifa mengine kuja hapa nchini. Baadhi ya
viongozi hao walitoka Ujerumani, Indonesia, Zambia, Jamhuri ya Kidemokrasia ya
Congo, Rwanda, Afrika Kusini, Falme za Kiarabu, Uswisi na Marekani. - Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kuratibu ziara za Viongozi Wakuu wa
nchi nyingine wanaozuru Tanzania ili kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia kati ya
Check Against Delivery
14
Tanzania na nchi nyingine. Ziara hizo zitaimarishwa ili nchi yetu iendelee kunufaika na
fursa za kiuchumi na kijamii lakini pia iweze kung’ara kikanda na kimataifa.
MAELEKEZO MAHSUSI
- Mheshimiwa Spika, wakati nikielekea kuhitimisha hotuba yangu naomba sasa
niweke msisitizo katika masuala muhimu yafuatayo ambayo ni uratibu wa upatikanaji wa
pembejeo; udhibiti na utatuzi wa migogoro ya ardhi; uhifadhi wa mazingira na
kuimarisha mazingira ya biashara.
Kuimarisha Uratibu wa Upatikanaji wa Pembejeo - Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuimarisha upatikanaji wa pembejeo
muhimu kwa wakulima zikiwemo mbolea. Hadi kufikia tarehe 31 Oktoba, 2023, wakulima
zaidi ya milioni 3.6 walikuwa wamesajiliwa na kupata namba za utambulisho za kununua
mbolea ya ruzuku. - Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kupitia Bunge lako tukufu kuwaelekeza
Wakuu wa Wilaya ambao pia ni Wenyeviti wa Kamati za Pembejeo za Wilaya
wawahamasishe wakulima kujisajili na kutoa taarifa sahihi kuhusu mazao wanayolima na
ukubwa wa mashamba yao kwenye madaftari ya wakulima ambayo yamesambazwa kwa
watendaji wa vijiji na mitaa ili taarifa zao ziweze kuingizwa kwenye mfumo na wapatiwe
namba za kununulia mbolea ya ruzuku. - Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kuielekeza Wizara ya Kilimo ihakikishe
mbolea inapatikana kwa wakati na ishirikiane na Wakuu wa Wilaya kusimamia kwa
karibu usambazaji wa mbolea kwa wakulima. Hatua hii iende sambamba na kutatua
changamoto zinazojitokeza wakati wa usambazaji wa pembejeo hiyo muhimu. - Mheshimiwa Spika, vilevile, kampuni na taasisi zinazozalisha mbegu bora
ziongeze kiwango cha uzalishaji na kuweka utaratibu mahsusi wa kufikisha mbegu hizo
kwa wakulima katika maeneo yao ya uzalishaji.
Udhibiti na Utatuzi wa Migogoro ya Ardhi - Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya
kushughulikia migogoro ya ardhi kwa kushirikisha Wizara za kisekta. Mikakati hiyo ni
pamoja na kuunda kamati maalum za kushughulikia migogoro, kuendesha kliniki maalum
za ardhi ambapo wananchi wamekuwa wakisikilizwa malalamiko yao na kupatiwa
ufumbuzi. - Mheshimiwa Spika, mikakati mingine inayoendelea kutekelezwa ni pamoja na
kufanya vikao na wadau mbalimbali kuhusu usimamizi bora wa ardhi; kufanya kaguzi za
milki; kutoa elimu kwa umma kuhusu utatuzi wa migogoro kwa kushirikiana na viongozi
Check Against Delivery
15
wa Serikali za Mitaa na kuwajengea uwezo watumishi ili kuimarisha huduma zitolewazo
kwa jamii.
- Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuwachukulia hatua watumishi
wanaochochea migogoro kwa kutozingatia sheria na kanuni na taratibu ikiwemo
kujihusisha na vitendo vya rushwa. Vitendo hivyo havikubaliki kwani ni kinyume na
maadili ya utendaji wa watumishi wa umma. Hivyo basi, nitumie fursa hii kumwagiza
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, kuwachukulia hatua kali watumishi
wa idara za ardhi wanaokiuka sheria. Hivyo basi, kila mmoja akafanye kazi kwa weledi,
uadilifu na kwa kuzingatia taaluma yake. - Mheshimiwa Spika, nilitoa maelekezo kwamba kampuni zote zilizopewa kazi za
upimaji wa viwanja kwenye Majiji, Manispaa na Mikoa na zimeshindwa kukamilisha kazi
hiyo, ziwe zilikuwa na mikataba ama hazikuwa na mikataba zichukuliwe hatua kali za
kisheria. Ikumbukwe kuwa, kampuni nyingi zilizopewa kazi za kupima maeneo ya
wananchi kwa lengo la kutoa hati miliki kote nchini hazifanyi kazi hizo kikamilifu licha ya
wananchi kulipa fedha kwa muda mrefu, nasisitiza kuwa kampuni hizo zikuchukuliwe
hatua za kisheria ikiwemo kuziachisha hizo. - Mheshimiwa Spika, nilielekeza pia kwamba, Halmashauri zote kama mamlaka
za upangaji ziongeze udhibiti na usimamizi wa maeneo ya wazi yaliyotengwa kwa ajili ya
matumizi ya umma na yale ya hifadhi ya mazingira, yakiwepo maeneo ya ukanda wa
kijani, maeneo ya wazi, viwanja vya michezo, makaburi na mengineyo ili kuzuia uvamizi
na mabadiliko ya matumizi ya maeneo hayo. Mfano halisi ni Jiji la Dodoma na Manispaa
ya Kigoma.
Maeneo yote yaliyotengwa na kuhifadhiwa yasiruhusiwe kufanyiwa mabadiliko ni vema
mabadiliko hayo yawe yamerishiwa na Kamati za Usalama za Mikoa na Wilaya kabla ya
kuwasilishwa kwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.
MICHEZO - Mheshimiwa Spika, kipekee nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa
Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa maono
mapana aliyonayo katika kuinua Sekta ya Michezo hapa nchini. Mheshimiwa Rais, katika
vipindi mbalimbali amekuwa akitoa miongozo ambayo imekuwa na tija na hatimaye
kuleta mapinduzi makubwa katika ya sekta ya michezo. Sina shaka mtakubaliana nami
kuwa kupitia maono yake, tasnia ya Michezo nchini inaendelea kuthaminiwa na
tumeendelea kushuhudia matunda mazuri kwa timu zetu zikiwemo zile za Taifa. - Mheshimiwa Spika, sote tunatambua kuwa ili timu zetu za taifa ziweze kushiriki
katika michuano ya kimataifa, maandalizi ya kutosha yanahitajika ambayo yanagharimu
fedha nyingi. Ninatoa pongezi kubwa sana kwa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya
Jemedari wetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano
Check Against Delivery
16
wa Tanzania kwa kufanya maamuzi sahihi ya kuiwezesha timu ya Taifa ya Tanzania
kufuzu katika Fainali za AFCON.
- Mheshimiwa Spika, aidha, Mheshimiwa Rais amekuwa akiridhia ujumbe
maalumu wa Serikali kuambatana na Taifa Stars katika michezo yao ya ugenini ili
kuongeza hamasa kwa wachezaji na matokeo kweli tumeyaona. Ninampongeza sana
Mheshimiwa Rais kwa kuendelea kutoa motisha kwa wanamichezo wetu ambazo
zimekuwa zikiongeza ari na hamasa kwa wanamichezo wetu. Licha ya kuendeleza
mpango wa Goli la Mama, mtakumbuka Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan mnamo
tarehe 4 Oktoba 2023 alinituma nikatekeleze ahadi yake ya kuwatunuku Timu ya Taifa
Stars fedha kiasi cha shilingi milioni 500 kwa kufuzu kushiriki mashindano ya Mataifa ya
Afrika (AFCON) yatakayofanyika nchini Ivory Coast Januari, 2024. - Mheshimiwa Spika, kwa upande mwingine, mafanikio katika sekta ya michezo
hapa nchini yamechagizwa pia michango ya Waheshimiwa Wabunge ambayo imekuwa
ikitolewa ili kuboresha sekta ya michezo nchini. Sote tu mashuhuda jamii sasa
imehamasika na ushiriki katika michezo na umeongezeka. Michezo imekuwa zaidi ya
burudani kwani sasa ni nyenzo muhimu ya kukuza uchumi kusaidia kutatua changamoto
mbalimbali katika Jamii ikiwemo ile ya ajira kwa vijana. - Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii pia kuwashukuru na kuwapongeza Baraza
la Michezo la Taifa (BMT) katika kutekeleza mikakati ya maendeleo ya michezo hapa
nchini Tanzania. Ushirikiano unaotolewa kwa taasisi za michezo umekuwa chachu ya
kufanikiwa kutimiza malengo yetu ya kuendeleza michezo.
Mfano mzuri ni ujenzi wa miundombinu ya kisasa ya Michezo kwa sekata ya umma na
binafsi. Kwa mfano Azam Complex, taasisi za ulinzi, taasisi za elimu kwa mfano shule,
vyuo na taasisi nyinginezo. - Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii pia kutoa pongezi nyingi kwa TFF kwa
uzinduzi wa Mashindano ya Ligi ya Soka ya Afrika uliofanyika Jijini Dar es Salaam tarehe
20 Oktoba katika Uwanja wa Benjamin William Mkapa ambao haujawahi kutokea. Katika
mechi hiyo ya uzinduzi Klabu ya Simba ilichuana na klabu ya Al Ahly ya Misri na kutoka
sare. - Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii pia kuipongeza sana Timu ya Taifa ya soka
ya Wanawake chini ya umri wa miaka 20 almaarufu Tanzanite Queens kwa ushindi wa
mabao 7 kwa 0 dhidi ya Djibouti katika mchezo wa kufuzu kombe la Dunia uliochezwa
Uwanja wa Azam Complex tarehe 11 Oktoba, 2023. Kwa ushindi huo, Tanzanite Queens
watachuana na Nigeria katika pambano litakalofanyika nchini Colombia mwaka 2024. - Mheshimiwa Spika, ninawapongeza pia timu ya Twiga Stars kwa kusonga mbele
katika hatua ya kufuzu mashindano ya WAFCON 2024. Ushindi huo umepatikana baada ya
kupata ushindi wa penati 4 kwa 2 baada ya kuifunga timu ya Ivory Coast kwenye
shindano lililofanyika pia katika Uwanja wa Azam Complex pale Chamazi Jijini Dar es
Check Against Delivery
17
Salaam. Aidha, ninawapongeza pia timu ya Twiga Stars kwa kufuzu mashindano ya
Olimpiki-2024 baada ya kuibwaga Botswana kwa bao moja bila katika mchezo uliofanyika
nchini Botswana.
- Mheshimiwa Spika, ninatoa pongezi nyingi kwa Timu ya wanawake ya JKT
Queens kwa kutwaa ubingwa wa Ligi ya Mabingwa Wanawake Ukanda wa Afrika Mashariki
na Kati (CECAFA). Ubingwa huo umewawezesha kushiriki Ligi ya Mabingwa ya Wanawake
Afrika inayoendelea nchini Ivory Coast. - Mheshimiwa Spika, licha ya mchezo wa mpira wa miguu, ninawapongeza pia,
vijana wetu Ramadhan Brothers wanasarakasi mahiri walioshiriki katika mashindano
maarufu ya American Got Talent. Vijana wetu hawa wameonesha vipawa na uwezo wa
hali ya juu katika mchezo huo na kukonga mioyo ya watazamaji wengi. - Mheshimiwa Spika, washiriki wetu katika mchezo wa ngumi wameendelea
kung’ara sana katika mashindano ya ndani na nje ya nchi yetu. Ninampongeza sana
Mwanamasumbwi wetu Ibrahim Class kwa kushinda mkanda wa TPBRC baada ya
kumshinda mpinzani wake Xiao Tau Su kutoka Jamhuri ya Watu wa China. - Mheshimiwa Spika, ninampongeza pia mwanasumbwi Pius Mpenda kwa
kushinda ubingwa wa WBC Peace Champion baada ya kumshinda Mrusi Dauren
Yeleussinov. Vilevile, ninampongeza sana Nahodha wa Timu ya Taifa ya Ngumi
Ngorongoro Black Rhinos Yusuf Lucas Changalawe kwa kufanikiwa kuingia katika fainali
ya mashindano ya Olimpiki ya Paris 2024. - Mheshimiwa Spika, kwa upande wa mchezo wa mashindano ya mbio,
ninampongeza sana mwanariadha wetu Magdalena Shauri kwa kushinda medali ya shaba
katika mbio za BMW Berlin Marathon baada kushika nafasi ya tatu katika mbio hizo.
Vilevile, ninampa pongezi nyingi Mwanariadha Alphonce Felix Simbu kwa kushika nafasi ya
pili kwenye mashindano ya majeshi yanayojulikana kama The World CISM Half Marathon
yaliyofanyika huko Uswisi. Ninawapongeza sana wanariadha wetu kwa ushindi huo
mkubwa. - Mheshimiwa Spika, nimpongeze pia Mheshimiwa Dkt. Damas Daniel Ndumbaro
(Mb.) Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo pamoja na watendaji wote wa Wizara kwa
kuendelea kusimamia vema utekelezaji wa maono ya Mheshimiwa Rais. Jitihada zenu
zinaonekana kwani Tanzania inazidi kung’ara katika medani za kimataifa. Sote
tunaendelea kushuhudia maendeleo makubwa ya sekta hii muhimu katika kuchangia Pato
la Taifa na kukuza uchumi kwa ujumla.
HITIMISHO - Mheshimiwa Spika, ninapoelekea kuhitimisha hotuba yangu, nitumie fursa hii
kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa kufanya mjadala wa Bunge hili kwa
kuzingatia manufaa makubwa ya ustawi wa taifa letu. Kama mnavyofahamu uwepo wa
Check Against Delivery
18
Bunge hili ulikuwa ni muhimu ili kuweza kupata maoni na ushauri kutokana na hoja za
Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali. Aidha ninawashukuru watumishi wa Serikali kwa
kuendelea kufanyia kazi masuala mbalimbali ambayo yamekuwa yakiwezesha uwasilishaji
wa hoja mbalimbali zilizotokana na mijadala ya Bunge hili.
- Mheshimiwa Spika, ninamshukuru Katibu wa Bunge na Watumishi wote wa
Bunge kwa huduma nzuri mliyotupatia katika kipindi chote cha Bunge hili. Kipekee,
nivishukuru vyombo vya ulinzi na usalama kwa kazi yanu nzuri, kwa maana tumeishi kwa
amani na utulivu katika kipindi chote cha Mkutano huu wa 13 wa Bunge la 12.
Ninawashukuru sana wanahabari kwa kuendelea kuuhabarisha umma juu ya shughuli zote
za Bunge letu Tukufu toka siku ya kwanza mpaka siku hii ya leo tunapoelekea kuhitimisha
mkutano wetu. Pia natambua mchango mkubwa wa huduma unaotolewa na madereva
wetu waliotuhudumia wakati wote. Pia ninatoa shukurani kwa watoa huduma wengine
mlioshiriki kutuhudumia muda wote tukiwa hapa Dodoma. - Mheshimiwa Spika, nirudie kukushukuru sana, wewe na Waheshimiwa Wabunge
wenzangu, niwaahidi kuwa tutaendelea kutekeleza yale mliyoyashauri na kuyatolea maoni
katika kipindi chote cha mkutano wa Bunge hili, kwani ushauri na maponi yenu ndio
msingi wa kuiwezesha Serikali kutimiza majukumu yake ipasavyo. Nami niwatakie
Waheshimiwa Wabunge wenzangu safari njema na mnaporejea majimboni kwenu na
mkaendelee kuwahakikishia wananchi dhamira njema ya Rais wetu Dkt. Samia suluhu
Hassan katika kuwaletea maendeleo Watanzania. - Mheshimiwa Spika, kwa kuwa tunaelekea mwishoni mwa mwaka, na hatutakuwa
na Mkutano wa Bunge tena ndani ya mwaka 2023, nitumie fursa hii kuwatakia Watanzania
na waumini wote wa Kikristo, sherehe njema ya sikukuu ya Krismasi na mwaka mpya wa
2024. - Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo, sasa ninapenda kutoa hoja kuwa
Bunge lako tukufu liahirishwe hadi siku ya Jumanne, tarehe 30 Januari, 2024 saa tatu
kamili asubuhi litakapokutana tena katika ukumbi huu hapa Jijini Dodoma. - Mheshimiwa Spika sasa ninaomba kutoa hoja.